Jumamosi, 19 Desemba 2015

Fasihi simulizi ya kiswahili na kiafrika



SWALI: Fasihi simulizi ya Kiafrika ni mfumo kamili wa elimu ya maisha ya watu. Kwa kutumia mifano, kutoka fasihi simulizi za jamii mbalimbali za Kitanzania. Jadili rai hii.


Dhana ya fasihi simulizi imeweza kutolewa fasili mbalimbali na wataalamu na wanazuoni mbalimbali, kutoka maeneo tofautitofauti. Fasili hizi mbalimbali zilizotolewa na wanazuoni na wataalamu wengi zimetokana na tofauti miongoni mwao katika mitazamo ya chimbuko la fasihi simulizi, kinadharia na matumizi ya fasihi simulizi kati ya jamii moja na nyingine kumepelekea kuwepo kwa fasili mbalimbali za fasihi simulizi kama ifuatavyo 

Mattelu, M.L., (1983:27) anafafanua kuwa fasihi simulizi ni aina ya fasihi ambayo hutumia mdomo katika kuumba, kuwasilishwa na kusambazwa kwa wasikilizaji na watumiaji wake. Anaendelea kusema kuwa fasihi simulizi ikiwa ni sanaa itumiayo maneno katika kutoa dhana fulani, hutegemea sana nyenzo mbalimbali za kuonekana na kusikika zitumiwazo na binadamu katika kujieleza.                                                                                                                       
Msokile, M (1992:3) fasihi simulizi ni kazi ya sanaa inayotumia lugha, kazi hii ya sanaa huhifadhiwa kwa kichwa na kusambazwa kwa njia ya masimulizi ya mdomo. Mwisho anaeleza kuwa fasihi simulizi imekuwa ikirithishwa kutoka kizazi hadi kizazi.                                                            Maelezo haya ya Msokile yanashabihiana na TUKI (2004) fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili.                                                                                                          Mazrui na Syambo (1992) wanasema fasihi simulizi ni sanaa ya matumizi ya lugha ya kubuni inayosambazwa kwa mdomo, kwa njia ya kuimba, kuchezwa, kuigizwa, kusimuliwa, kuumba, kufumbua au kutegua mafumbo ya vitendawili.                                                                                Pia naye Mulokozi, M.M (1996) anasema, fasihi simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi.                                                                                                                                                         Baada ya kuangalia maoni mbalimbali ya wataalamu hao, tunaweza kuhitimisha kwa kusema kuwa fasihi simulizi ni aina ya fasihi inayowasilishwa kwa hadhira kwa njia ya masimulizi ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi, na hurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.                                                                                                                                                         Fasihi simulizi ya Kiafrika ni ile fasihi ambayo kwa asili yake imechimbuka na kuibuliwa na Waafrika wenyewe na huwasilishwa kwa njia ya mdomo kwa kusimuliwa, kuimbwa, kutongolewa au kughaniwa. Fasihi hii ina mawanda mapana kwani hujumuisha jamii zote za Kiafrika na makabila yote ya Kiafrika kama vile Wabuganda kutoka nchini Kenya, Wazulu kutoka Afrika Kusini, Kikuyu kutoka nchini Kenya, Wakinga, Wabena, Wapare, Wasukuma kutoka nchini Tanzania.                                                                                                                             Pia fasihi hii hujumuisha lugha mbalimbali za kiafrika, tamaduni zao, nyimbo zao, mila na desturi zao kama vile matambiko , jando na unyango, kwa mfano kabila la Wakinga linalopatikana mkoani Njombe nchini Tanzania wanamsitu wao ambao watu wa kabila hili huenda kuomba kutatuliwa matatizo yao, shida na shukurani kwa mungu wao, msitu huo unaitwa Nyumba nitu.                                                                                                                                                 Ni kweli kabisa fasihi simulizi ya kiafrika ni mfumo wa elimu ya maisha ya watu. Kauli hii inaweza kufafanuliwa zaidi kwamba, ndani ya fasihi simulizi ambapo kuna tanzu na vipera mbalimbali vinavyotendwa na wasanii katika jamii huchochea na kuhamasisha ujifunzaji, uelewaji na kuongeza maarifa katika mfumo mzima wa maisha ya mtu au jamii. Kupitia vipengele mbalimbali vya fasihi simulizi kama vile nahau, nyimbo, vitendawili, soga, ngano, tendi, mashairi, majigambo, ngonjera, visasili, na tarihi, vimekuwa kama darasa katika kuleta elimu ya maisha ya watu ndani ya jamii katika kuendesha maisha yao.                                                            Fasihi simulizi huendana na muktadha katika utendaji wake, kama asemavyo Mulokozi, M.M. (1996: 24) kuwa fasihi simulizi ni tukio linalofungamana na muktadha fulani wa jamii na kutawaliwa na mwingiliano wa fanani, hadhira, fani inayotendwa, tukio, mahali na wakati.           
   Hivyo basi, fasihi simulizi ya kiafrika ni mfumo kamili wa elimu ya watu katika muktadha fulani katika jamii fulani, katika shughuli zao za kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii kwa sababu zifuatazo:                                                                                                                        
           Kufunza jamii: Fasihi simulizi ya Kiafrika hupelekea mafunzo juu ya maisha ya ndoa. Katika kipengele hiki, vijana waliweza kupata mafunzo ya ndoa kabla ya kuanza maisha ya ndoa. Kwa mfano, Suala la ndoa katika kabila la wasafwa wanaopatikana wilaya ya Mbeya, mkoani Mbeya waliohusika kumfundisha mwali ni shangazi na bibi ambao hasa walikuwa ndio fanani, mwali huyo alifundishwa namna ya kuishi katika ndoa pamoja na matumizi mazuri ya chakula katika familia, kwa mfano binti alifundishwa kupika chakula ambacho kingetosheleza mahitaji ya mumewe na familia yake kwa ujumla bila kubakiza na kukitupa. Katika shughuli hii mwali ndiye aliyekuwa hadhira na ukweni ndio palikuwa mahali pa kutendea na maudhui yalikuwa ni mafunzo kuhusu maisha ya ndoa na fanani walikuwa bibi na shangazi wa mwali, katika kipindi hicho mafunzo hayo yalimfundisha mwali namna ya kuishi na jamii inayomzunguka na mafunzo yote yalifikishwa kwa njia ya misemo, nyimbo na hadithi. Mfano wa nyimbo zilizokuwa zikiimbwa wakati wa mafunzo hayo ni kama vile:
                                         “Wamala yashi ingano
                                           yaleta bana yao
                                           yenye ubaba ni mama
                                           bayinzilile mwigomba”.
Wimbo huu ulimfundisha mwali kutokumaliza chakula ndani kwa ajili ya matumizi ya baadaye na kwa ajili ya wageni. Pia katika kabila la Wanyakyusa lililopo mkoani Mbeya wilaya za Rungwe, Busokelo na Kyela, mabinti walipewa mafunzo na shangazi pamoja na bibi. Shangazi na bibi waliwafunza mabinti zao namna ya kupika chakula cha kutosha familia, kumtunza mwanaume, kuheshimu wakwe na jamii nzima, kufanya kazi na kulea  watoto vizuri. Ndani ya mafunzo haya, shangazi na bibi walikuwa fanani, binti alikuwa ndiye hadhira na ukweni ndio mahali. Wanyakyusa waliweza kuimba wimbo ufuatao:
                                                Mwanetu                                                                                                                                              ukulile                                                                                                                                                  Bhombaga imbobo                                                                                                                                kundumegho
Tafsiri yake                                                                
                                                 Mtoto wetu                                                                                                                                         umekua                                                                                                                                                fanya kazi                                                                                                                                            kwa mumeo 
Kabla ya utandawazi, fasihi simulizi katika jamii ya Kinyakyusa na Kisafwa zilifunza mabinti na kusaidia maisha yao ya ndoa kuwa salama, tofauti na wakati huu wa Harusi na Kitchen Party (sherehe za kumuaga binti anaeolewa) ambapo vijana hawapewi elimu ya kutosha.                                                              
            Kuonya na kukosoa jamii, zipo tanzu na vipera mbalimbali vya fasihi simulizi ambavyo hujihusisha zaidi na kuiweka jamii katika nafasi iliyobora zaidi. Mfano; kimaadili kuna methali zinazoonesha maadili mema katika jamii mfano; “Samaki mkunje angali mbichi”, “Mkaidi hafaidi mpaka siku ya iddi”. Vilevile kiuchumi zipo methali ambazo huonya na kukosoa wale wote wenye tabia za kivivu katika kujitafutia maisha mfano, “Mtegemea cha ndugu hufa masikini”,Fanya  kazi kama mtumwa uishi kama mfalme”. Pia kupitia hadithi mbalimbali ambazo husimulia zimekuwa ni msaada mkubwa kwa jamii, kwani zimekuwa zikionya na kukosoa jamii, kwa mfano, kabila la wanyakyusa walikuwa wakisimulia hadithi ifuatayo kwa lengo la kuonya na kukosoa watu ambao walikuwa hawataki kusikia ushauri wa wazazi.
                                                    Kapango kapango:
Ijolo alipo bhabha jumo alinumwana unyambala bho akulile kafikile  akabhalilo ka kwegha, bhabha ghwake alimbulile ukuti atikulondighwa ukwegha kutali,(ikikolokyapanja)ghwegheghe unyakyusa,lelo umwene akanile ukwegha unyakyusa abhukile ikikolo kyapanja, bhoafikile munjila alimwaghile undindwana jumo bhalina mama ghwake pasi pa mpiki pakaja pa myabho.Alinganile nukulonda ukumwegha,bho alalusisye ifyuma, mama jula atile ungasosya ifyuma nafimo loli kumpimba mpaka kumyenu. Loli bhobhafikile munjila undindwana jula akanile ukusuluka alyandile ukwimba”
             “ Ghwali nyeghile kumyitu x2
              ikisu kya kutukuju kumyetu kula kula x2”
Pitasi unyambala jula alambalele nu ndindwana jula pa nyuma ngimba akalimundu lyali setano. Lyali ngoghile nukwega indumbula jake, undumyana jula alinkwenda nu kufwa.

Tafsiri yake kwa lugha ya Kiswahili;
                                                               Hadith hadithi:
Hapo zamani za kale palikuwepo na baba mmoja aliyekuwa na mtoto wa kiume. Alipofikia umri wa kuoa baba yake alimwonya kuwa sheria ya Kinyakyusa hairuhusu kuoa nje ya kabila lao lakini yeye alikataa akaondoka kwenda nje ya kabila lake. Alipofika njiani alimkuta binti mmoja na mama yake wakiwa chini ya mti nyumbani kwao. Akampenda yule binti na kuridhia kumuoa. Alipouliza kuhusu mahari yule mama akasema asitoe kitu chochote ila kumbeba hadi nyumbani kwake. Lakini walipofika nyumbani yule binti alikataa kushuka na kuanza kuimba.
      “ulinitoa kwetu x2
        Kaniweke kwangu mji wa Tukuyu, kule kwetu kule x2
Kijana yule baadaye aliamua kulala huku binti akiwa mgongoni. Kumbe hakuwa binti bali ni jini likamuua kwa kumtoa utumbo na ikawa mwisho wa maisha ya yule kijana.

Pia kabila la Wakinga, nao walikuwa na wimbo ambao ulikuwa unatoa maonyo na kukosoa watu wanaotenda matendo ambayo ni kinyume na sheria na kanuni za jamii.

                                    Okhiweni ulukhi pakhiholo ove jova X2                                                                                            wita livava lyong’a ove jova khombe,                                                                                                 witaka omwana we jova X 2
Tafsiri yake
                                    Umeona nini mtoni wewe mama X 2                                                                                                  Unasema unaumwa kiungolila kumbe                                                                                                Unatupa mtoto we mama X 2
Wimbo huu unawaonya na kuwaasa wanawake na wasichana kuwa wasitoe mimba wala kutupa watoto kwani mtoto ni hazina na msaada siku za mbeleni kwani hujui ukizeeka nani atakusaidia (atakayekuzika).                                                                                                                                              Kuchambua na kuchochea umma, kuwafumbua macho, kufichua uozo au uchafu uliomo katika jamii, wasanii wa fasihi simulizi hutunga kazi zao ambazo huwafumbua macho watu kwa kufichuo uozo na maovu yaliyoka katika jamii, kama vile uongozi mbaya, umbea, usaliti, unafiki, wizi, uongo, mila potofu na unyanyasaji wa kijinsia. Kwa mfano, wapo wasani mbalimbali ambao huimba nyimbo ambazo huchambua na kuchochea umma, kuwafumbua macho, kufichuo uozo na uchafu uliomo katika jamii, baadhi ya wasanii hao ni kama Mrisho Mpoto wimbo wake wa Chochea kuni na Mjomba ni nyimbo ambazo zimebeba maudhui ya kufichuo uozo uliomo katika jamii kama vile uongozi mbaya, usaliti, matabaka, hali ngumu ya maisha ya watanzania na unyonyaji. Pia, msanii Roma ana nyimbo ambazo hufumbua macho jamii, nyimbo hizo ni kama Mr. President, Tanzania, Viva Roma hizi ni nyimbo ambazo zimechochea umma wa watanzania na kuwafumbua macho juu ya mwenendo wa siasa na maisha, uongozi mbaya na usaliti. Pia msanii kutoka Afrika Kusini marehem Luck Dube kupitia nyimbo zake za Together as one na Different colours ziliwafumbua macho Waafrika kuungana ili kujikomboa kutoka mikononi mwa wakoloni, na pia nyimbo zake zilikuwa na maudhui ya kupinga ubaguzi wa rangi.                                                                                                                              Huleta ufahamu juu ya amali na utamaduni wa jamii husika. Fasihi simulizi ya Kiafrika hupelekea kuleta ufahamu juu ya amali za jamii husika, mila na desturi, tamaduni, maadili na hekima ndani ya jamii. Kutokana na fasihi simulizi ya watu wa jamii fulani huishi kwa kufuata miiko, mila na desturi za mahali hapo. Kutokana na tamaduni hizo kunakuwa na amali ya kutosha inayowafanya watu hao waishi kwa furaha na kufanya shughuli zao za kimaendeleo. Kwa mfano, katika jamii ya Wanyakyusa mabinti waliweza kuishi kwa kujitunza ili waweza kutunza mila na desturi za Kinyakyusa, mabinti waliishi kimaadili bila kuingiliwa kimwili yaani wasipoteze “ubikra wao” kwa binti aliyepoteza ubikra aliitwa “bhalile inguku” yaani “hamna au wamekula wakuku” wakiwa na maana “hana bikra”. Binti huyo alitolewa mali chache (ng’ombe) na kuonekana hafai katika jamii, pia amewadhalilisha wazazi wake. Hivyo mabinti waliishi kwa kuogopa kuingia katika mahusiano ya kimapenzi katika umri mdogo ama kabla hajaolewa. Binti aliyeolewa akiwa na bikra alitolewa mali nyingi na alileta heshima kubwa kwa wazazi wake. Pia kuna nahau mbalimbali za Kiswahili ambazo hutumika kutoa maadili na kuonesha utamaduni wa jamii husika mfano:
                                                Achiwa mkopa                                                                                                                                                maana yake: Rithishwa kazi ya uganga          
                                                Chinja kafara                                                                                                                                      maana yake: toa sadaka                     
Nahau hizi zilitumika sana katika jamii nyingi za Waswahili, kwa lengo la kutoa maadili na kuendeleza amali na utamaduni wa jamii.                                                                                        Kuhimiza kazi: Fasihi simulizi ya Kiafrika ilihimiza sana kazi na hii elimu ilitolewa wakati wa jando na unyango.  Jando na unyago ni sehemu ya malezi yanayolenga kumsaidia mtoto kukabili vema hali yake ya kuwa mwanaume au mwanamke ili jinsia imjenge badala ya kumvuruga. Mara nyingi wavulana huwa wanaongelea siri zao zinazowahusu wao katika makuzi yao na huwa hawataki mtoto wa kike kuzijua hali kadhalika kwa upande wa mtoto wa kike nao huwa wana mafunzo yao ambapo nao huwa hawapendi mambo wanayojifunza yajulikane kwa watoto wa kiume, mafunzo haya yaliweza kutolewa na watu wazima ambao ndio walitegemewa zaidi na jamii katika kutoa elimu ya jinsia. Katika jamii za kibantu zilikuwa na kawaida ya kuongelea mafunzo hayo ya siri na wazee hasa babu na bibi ndio walihusika sana katika kutoa mafunzo hayo, kulikuwa na mafundisho rasmi ambayo yalikuwa na umuhimu wa kujua mapema ukweli hasa kuhusu maumbile ya binadamu. Kadri mtoto anavyozidi kukua ndivyo alivyohitaji kujifahamu kijinsia ili aweze kukomaa na hatimaye kukabiliana na shughuli mbalimbali za kijamii. Kwa  mfano, Katika kabila la Wanyakyusa walizingatia malezi ya vijana na ilikuwa ni mwiko kwa mtoto wa kinyakyusa kudeka, mama aliweza kula na watoto wa kiume chini ya miaka kumi pamoja na wale wa kike ambao walikuwa bado hawajaolewa, lengo kubwa ilikuwa ni kuwafundisha kula kwa adabu na kuheshimiana. Kwa upande wa mtoto wa kiume aliruhusiwa kukaa na mama yake akiwa na umri chini ya miaka kumi, baada ya umri huo hakuruhusiwa kukaa tena na mama yake bali aliambatana na wanaume kwa lengo la kujifunza kazi. Mgawanyo wa kazi ulizingatia umri na jinsi kwa kuwa zamani watoto wengi hawakuwa na fursa za kusoma, hivyo walipata elimu (mafunzo) kutoka kwa wazazi wao. Watoto walipofikisha umri wa miaka kumi na moja au kumi na mbili waliweza kukusanywa kutoka familia tofauti na kupelekwa mbali na wazazi wao ili kujifunza maisha na kujitegemea na hivyo kuweza kuanzisha vijiji vipya kwa kujenga nyumba kisha kuanzisha familia.
Wakati wa utoaji wa mafunzo hayo semi na nyimbo mbalimbali zilitumika na zilitolewa na wazee, kwa mfano:
                                           “ Ukukoma ingunguni”
             Tafsiri yake ni;        “Kuua kunguni” 
Msemo huu ulilenga kuelimisha watoto na kuwakomaza kuwa kuendelea kuishi kwenye nyumba ya wazazi pamoja nao na hali wakiwa wamefikia umri wa kujitegemea sio vizuri, hivyo walisisitizwa zaidi kujitegemea. (Mwambusye, 2012:23).
                                              “Ukukula kitalikitali
             Tafsiri yake ni;     “Kukua haraharaka lakini bila umbile na akili au hekima”.
Katika msemo huu walimaanisha zaidi kuwa mwili unakua upesi kuliko akili yaani ukuaji wa mwili hauendi sambamba na ukuaji wa akili (Mwambusye, 2012:27).
Kutokana na mafunzo haya ya kukaa pamoja, vijana waliweza kujifunza majukumu mbalimbali na malezi ya jamii zao kwa ajili ya maendeleo ya pamoja na kuhimiza ushirikiano, kuheshimiana na kuthaminiana na hatimiye kuishi kama ndugu na jamii moja na hapo ndipo  Wanyakyusa wanapo sema:
                                            “Nkamu ju mundu
                 Tafsiri yake ni:   “Undugu ni kufaana na sio kufanana”.
Pia kuna methali ya Kiswahili inayosema Mgagaa na upwa hali wali mkavu, methali hii inahimiza wanajamii kufanya kazi kwa bidii ili kukidhi mahitaji yao. Hivi ndivyo fasihi simulizi ya kiafrika ilivyokuwa ikihimiza masuala ya kazi, kufanya kazi kwa bidiii.                                                          Kuipa jamii mwelekeo. Kwa kuelimisha na kuyapitisha mawazo yanayohusiana na jamii fulani, wanajamii wanahakikisha kuwa jamii imepata mwelekeo. Katika vitanzu vya fasihi simulizi huwako na adili na ujumbe ambao unawaelekeza, kuwaadibu, kuwaonya na kuwaongoza kwenye matarajio mema ya jamii husika. Kwa mfano, katika jamii nyingi, fasihi simulizi ilitumiwa kama njia ya kuwaelekeza na kuwafundisha vijana mwenendo mzuri, maadili yafaayo pamoja na falsafa ifaayo katika jamii. Kwa mfano, jamii ya Waswahili, Unguja na Pemba huimba sana wimbo ufuatao lengo lilikuwa kuwatia moyo vijana.
                                    Mwanangu amba duni hino,                                                                                                               Ndo urume                                                                                                                                          Mrume hujikaza mrume                                                                                                                       Mrume mwana hujikaza mrume
                                   
Mume wangu mwanao alia                                                                                         Memeze ngariba kamchachia

Mwanangu ukubwa una raha                                                                                     Hili shida uje uone                                                                                                           Mwanangu shika mndu na msaha                                                                          Uchimbe shimo wasivione                                                                                          Ruka ukijitoa tunawe                                                                                                   Mwana wa hali ni watu wenyewe

            Kuhimiza umoja na mshikamano, fasihi simulizi ya kiafrika huhimiza jamii kuwa na mshikamano ili kuleta maendeleo katika jamii zao. Kwa mfano methali ya Kiswahili inayosema kidole kimoja hakivunji chawa, umoja ni nguvu utengano ni udhaifu. Methali hizi husisitiza suala la umoja na mshikamo miongoni mwa wanajamii. Pia, Katika kabila la Wanyakyusa na Wasafwa wana namna moja katika kushirikiana wakati wa misiba na matatizo mbalimbali kwa mfano, ukitokea msiba katika familia fulani kwenye jamii, jamii nzima huhusika katika msiba ule na kushirikiana katika shughuli zote za msiba huo. Wanaume na wanawake wa jamii nzima waliwajibika kushinda na kulala mahali palipotokea msiba na kila mmoja katika jamii huweza kuchangia chakula, kuni na vifaa vingine vilivyotumika katika shughuli nzima ya mazishi kama vile majembe, makoleo, mkeka na ng’ombe, hii ilikuwa ni kulingana na uzito wa msiba uliokuwa umetokea. Mbolezi ziliimbwa wakati wote wa msiba ambapo waghani walikuwa wakitaja sifa na mema ya marehemu au ukoo wa marehemu, waombolezaji wengine waliimba na kupita sehemu mbalimbali za makazi yao wakiimba na kuchangishana nafaka kwa ajili ya msiba, kwa mfano katika kabila la Wasafwa walikuwa wanaimba nyimbo kama hizi:
                                       “Kiongozi:     Ndio maana ×2
                                        Waitikiaji:   Ndio maana twinzile      
                                        Kiongozi:     Ndio maana ×2
                                        Waitikiaji:   Ndio maana twinzile
                                        Kiongozi:     (Hutaja jina la marehemu au ukoo wake)
                                        Waitikiaji:   Ndio maana twinzile”.
Tafsiri yake
                                    Kiongozi: Ndio maana x 2                                                                                                                Waitikaji: Ndio maana tumekuja                                                                                                        Kiongozi: Ndio maana x 2                                                                                                                       Waitikiaji: Ndio maana tumekuja                                                                                                          Kiongozi: (Hutaja jina la marehemu au ukoo wake)                                                                              Waitikiaji: Ndio maana tumekuja”.

Wimbo huu hutumika kuonyesha uhusiano mzuri kati ya jamii na ndugu pamoja na jamaa waliofiwa, wimbo una maana kuwa (Tumekuja kwa sababu tunaushirikiano na nyie).
Kwa upande wa kabila la Wanyakyusa waliimba hivi:
                                       “Kiongozi:   Twalimenye naloli           
                                        Waitikiaji:  Twalimenye naloli
                                         Kiongozi:   Ukete abhandu bikulila
                                         Waitikiaji: Ukete abhandu bikulila
                                         Kiongozi:  Keta tukwenda tukulila
                                         Waitikiaji: Keta tukwenda tukulila”
Tafsiri yake:
                                       “Kiongozi:  Tulimjua sana       
                                        Waitikiaji: Tulimjua sana
                                        Kiongozi:   Ona watu wanavyolia
                                        Waitikiaji:  Ona watu wanavyolia
                                        Kiongozi:   Tazama tunatembea tukilia
                                        Waitikiaji:  Tazama tunatembea tukilia”.

Nyimbo hizi ni za maombolezo na zilikuwa zikiimbwa wakati wa msiba, wanajamii waliimba kwa lengo la kumkubuka marehemu au ndugu yao aliyewatoka.                                                    Kwa ujumla, fasihi simulizi ni zao la jamii na inafungamana na maisha ya watu. Fasihi simulizi inazungumzia juu ya mwanadamu na mazingira yake. Kukua kwa sayansi na teknolojia ni sehemu muhimu sana katika kuleta maendeleo katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni ambapo maendeleo ya sayansi na teknolojia yamesababisha utandawazi. Kutokana na mabadiliko haya, fasihi simulizi kama kazi ya kisanaa iliyojaa ufundi na ubunifu ndani yake haina budi kuendana na mabadiliko hayo maana hata mfumo wa maisha hubadilikabadilika katika jamii kulingana na maendeleo yanavyozidi kuimarika na kujitokeza. Hivyo pamoja na mabadiliko hayo si vyema kupuuza fasihi simulizi kwani yenyewe ndiyo fasihi kongwe na ndiyo iliyoibua fasihi andishi baada ya kugundulika kwa maandishi kwani fasihi hata kabla ya utandawazi ilikuwa na mchango mkubwa sana katika kuimarisha na kutoa elimu kwa jamii.


                                     





                                          MAREJEO

Msokile, M. (1992). Misingi ya Hadithi Fupi. Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press.

Mulokozi, M.M. (1996). Utangulizi wa Fasihi Simulizi ya Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI.
Syambo, B. na Mazrui, A. (1992). Uchambuzi wa Fasihi. Nairobi: EAEP.
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam: TUKI.

Wamitila, K.W (2003). Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi.Nairobi: Focus Publications Ltd.
Wamitila, K.W. (2002). Uhakiki wa Fasihi: Misingi na Vipengele Vyake. Nairobi: Phoenix Publishers.

Jumamosi, 3 Mei 2014

NADHARIA KUHUSU CHIMBUKO LA FASIHI SIMULIZI

  1. NADHARIA KUHUSU CHIMBUKO LA FASIHI SIMULIZI

Chanzo na Chimbuko la fasihi simulizi                                                                                            Wataalamu wa fasihi simulizi, wamezuka na nadharia kadha kuelezea asili, chanzo, chimbuko, ukuaji na ueneaji wa fasihi simulizi. Kuna nadharia kuu tatu zinaelezea kuhusu chimbuko na chanzo cha fasihi simulizi, ambazo ni:
1.      Nadharia ya kiulimwengu (utandawazi), imegawanyika katika sehemu tatu, ambazo ni:   - Ubadilikaji
- Msambao
- kisosholojia
2.      Nadharia ya utaifa
3.      Nadharia ya hurutishi

1. Nadharia ya Kiulimwengu (Utandawazi)                                                                                     Hii ndiyo nadharia ya kwanza kuelezea kuhusu chimbuko na chanzo cha fasihi simulizi. Watafiti wa nadharia hii walikuwa wazungu wa Ulaya, hivyo nadharia hii iliegemea zaidi mtazamo wa Kimagharibi. Mawazo ya nadharia ya kiulimwengu yamegawanyika katika makundi matatu:
(a) Ubadilikaji Taratibu                                                                                                                            Muasisi wa nadharia hii ni Charles Dawin (1809-1882), na wafuasi wake waliamini kuwa kuna misingi anuai kuhusu kanuni zinazoongoza asili na maendeleo ya utamaduni wa mwanadamu. Kundi hili liliona kuwa dhana ya ubadilikaji taratibu misingi yake mikuu ni viumbe hai. Wanasema viumbe hai vyote vinakuwa katika mchakato wa mabadiliko mbalimbali hadi kufikia kwenye maumbo yao ya sasa. Hivyo na fasihi simulizi imepitia michakato mingi ya mabadiliko mpaka kufikia katika umbo lake la sasa, mfano fasihi simulizi ya kipindi cha Ujima ni tofauti na fasihi iliyofuata katika vipindi vingine kama vile wakati wa Utumwa, Ubepari hata mfumo tulionao sasa.                                                                                                                            Hivyo, fasihi similizi ya kiafrika hubadilika kutoka kipindi kimoja hata kingine kutokana na mabadiliko ya kijamii. Kwa ujumla waasisi hawa wanaamini kuwa chimbuko la fasihi simulizi ni jamii yenyewe na kutokea kwa kufanana kwa kazi za fasihi simulizi kutoka jamii moja hadi nyingine kunasababishwa na hatua sawa za mabadiliko kiakili na kijamii kwani jamii moja iliyozagaa ulimwenguni kote akili zao ni sawa.                                                                                                                           
Dosari ya nadharia hii ni kwamba waliziona kazi za fasihi simulizi za Kiafrika kwamba hazina mwenyewe kwa kuwa ni mali ya jamii nzima. Walisema kwamba, ijapokuwa fasihi simulizi ni mali ya jamii, lakini sio kwa kiwango hicho walichokisema wao. Walisisitiza kuwa si kila mzungumzaji anaweza kuwa fanani wa fasihi simulizi. Wao walilipuuza suala la upekee wa muktadha.

Ubora wa nadharia ya kiulimwengu (kitandawazi)          
Ø  Mchango wao katika nadharia ya fasihi simulizi, umechangia kuibuka kwa nadharia nyingine zinazoeleza kuhusu chanzo na chimbuko la fasihi simulizi.
Ø  Wanakubali kwamba Afrika ilikuwa na fasihi simulizi.
Ø  Waliweza kubaini baadhi ya tanzu za fasihi simulizi, mfano hadithi za kale, methali, vitendawili, jado na unyago, kusalia miungu, mivigha, n.k.

Udhaifu wa nadharia hii
Ø  Mtazamo huu ulikuwa wa kimagharibi zaidi, hivyo,waliegemea zaidi utamaduni wa Ulaya.
Ø  Walijikita zaidi kuelezea historia ya utamaduni wa Kiafrika na kusahau kutafiti kazi za fasihi simulizi.
Ø  Nadharia zao zilikuwa za kufikirika zaidi, hivyo ni vigumu kuzithibitisha kisayansi.
Ø  Walisisitiza zaidi mfanano kana kwamba jamii hizi hazikuwa hazina tofauti yoyote katika kazi zao.

(b) Msambao                                                                                                                                      Waasisi wa nadharia hii ni Grimms na Thompson. Wanamsambao wamepingana na wanaubadilikaji taratibu ambao (wanaubadilikaji taratibu) waliamini kuwa kufanana kwa fani mbili za kifasihi kunatokana na jamii hizo kupitia hatua sawa za kimaendeleo, wanamsambao  wanaamini kuwa pale ambapo kufanana kwa namna hiyo kutatokea sababu ya msingi ya mfanano huo ni kuwa katika kipindi fulani hapo zamani jamii hizo ziliwahi kukutana kwa namna fulani na makutano hayo yalisababisha hali ya kuazimana baadhi ya mila na desturi.                   Kwa ujumla mawazo ya wafuasi wa nadharia hii wanaamini kuwa utamaduni unaweza kusambaa kutoka katika jamii imara, yenye nasabu bora, jamii iliyostaarabika na maarufu tena yenye nguvu kuelekea katika utamaduni wa jamii iliyo dhaifu au duni. Hivyo basi kutokana na mawazo ya wataalamu hawa ni kuwa fasihi simulizi ya kiafrika ilisambaa kutoka katika sehemu moja iliyostaarabika (Ulaya) kwenda sehemu nyingine ambayo haijastaarabika (Afrika). Kwa mfano, ushairi wa simulizi wa kiswahili ulitoka Uarabuni na Uajemi kuja Afrika na huko ndiko ambako kulionekana kuwa kumestaarabika kuliko Afrika na ndiyo maana ushairi huo uliletwa huku Afrika.                                                                                                                                            
 Dosari ni kwamba, wananadharia hii wanaamini kuwa chimbuko na asili ya fasihi simulizi ya Kiafrika ni Ulaya, jambo ambalo hatuwezi kukubaliana nalo kwani kila jamii ina fasihi yake na kutokea mfanano wa baadhi ya kazi za fasihi huenda kuna kuathiriana kwa namna fulani miongoni mwa jamii hizo.                                                                                                                              
 Dosari nyingine ni kwamba, si kweli kuwa jamii duni, isiyostaarabika au zinazoendelea hazina fasihi yoyote, kama walivyodai wana nadharia hii. Upo ushahidi unaothibitisha kwamba lugha za Kiulaya na fasihi yake zimeiga (zimeathiriwa) mambo ya Kiafrika, kwa mfano, neno shamba, ugali, mama katika Kiingereza ni wazi yametoka katika lugha za Kiafrika, hususan Kiswahili; pia uchezaji wa kukata viuno Ulaya si asili yao, hasa ni utamaduni wa Kiafrika, mavazi ya khanga na kadhalika. Aidha hawatoi ushaidi wa kisayansi wa uduni wa bara la Afrika.                                  
 Pia, wanamsambao walisisitiza zaidi ufanano na kupuuza tofauti. Kwao walieleza ufanano kana kwamba jamii hazikuwa na tofauti yoyote katika kazi hizo za fasihi. Kwa kuwa jamii hizi ziliishi katika mazingira tofauti na zilikuwa na kiwango tofauti cha maendeleo, ilikuwa wazi kwamba kulikuwa na tofauti pia.

(c) Nadharia ya Kisosholojia                                                                                                          Sosholojia ni taaluma inayochunguza mfumo wa kijamii, yaani mahusiano ya wanajamii, mfumo wa kiutawala wa kijamii, maendeleo ya kijamii na kadhalika. Baada ya kugundua kuwa nadharia ya ubadilikaji taratibu na msambao zina mapungufu, ndipo nadharia hii ikaibuka. Nadharia hii ya kisosholojia ina mihimili mitatu ambayo ni ule wa Umahususi na sio umajumui, mkazo katika utendaji na mhimili unaosisitiza dhima ya fasihi simulizi katika jamii.
\
Umahususi
Kwa kuanza na mhimili wa Umahususi, nadharia hii ilijikita zaidi katika jamii peke yake badala ya kujikita katika taaluma ya sanaa jadi kwa ujumla kama walivyofanya wananadharia wa nadharia ya kiutandawazi. Hii ilikuwa baada ya kugundua dosari zilizofanywa hapo kabla, Dosari ya kutoa tamko la juu juu na la jumla zaidi ambapo matamko hayo mara nyingi yalitupilia mbali vipengele fulani vya lugha na mienendo mingine ya jamii.

Mhimili wa utendaji
Pia katika mhimili wa utendaji, Wanasosholijia waliweka msisitizo katika kuchunguza utendaji (performance) wa kazi mbalimbali ya fasihi simulizi. Kutokana na msisitizo huo imebainika kuwa fanani wa kazi ya fasihi wanaujuzi na ustadi wa kiutendaji katika sanaa husika na jambo hili limetuwezesha kuelewa kuwa katika fasihi simulizi kuna kipengele cha utendaji. Vilevile  wamedokeza sifa za ndani za fasihi simulizi ya kiafrika, na hivyo wao wanaona kuwa ili kujua fasihi simulizi ya kiafrika ni vyema kuangalia jamii na utendaji wa kazi husika.

 Dhima ya fasihi simulizi katika jamii
 Katika msisitizo juu ya dhima ya fasihi simulizi katika jamii, Wanasosholojia wanaamini kuwa uamilifu wa fasihi simulizi upo hai na haufi na kwamba unabadilika kulingana na maendeleo ya jamii husika.
Hivyo ili kuelewa historia ya fasihi simulizi kutokana na mawazo ya wanasosholojia ni wazi kwamba unapaswa kuangalia jamii husika, utendaji na dhima ya fasihi katika jamii husika, kwani mihimili hii ndiyo chanzo au historia ya fasihi simulizi ya jamii husika. kutokana na mawazo ya wananadharia hii ni wazi kwamba asili ya fasihi simulizi ya kiafrika ni ndani ya jamii za Kiafrika zenyewe na si vinginevyo.                                                                                                               Dosari ya nadharia hii ni kwamba ingawa walijitahidi kuipa hadhi kwa kusisitiza upekee wa muktadha wa kijamii wa fasihi simulizi ya Kiafrika tofauti na waliotangulia hawakuchunguza kwa undani sifa za kisanaa za fasihi simulizi. Wameandika ngano kwa namna ya kupwaya, hazivutii. Wameshindwa kuchambua sanaa kubwa iliyomo kwenye matini chanzi nyingi za kifasihi simulizi walizochunguza (uradidi, mishtuko, wombo, n.k.). Hivyo basi, haikuwa rahisi kuuona ufasihi kwa ujumla wake kutokana na tafiti za kisosholojia kwasababu fasihi ni sanaa na hubebwa na fani na maudhui.   

2.NadhariayaUtaifa                                                                                                                                     
Nadharia hii ilizuka kwenye vugu vugu la kudai Uhuru Barani Afrika. Wanautaifa  wanadai kuwa wananadharia wa nadharia ya ulimwengu hawakuwa  na uelewa wa kutosha kuhusu lugha za kiafrika, Kwa kiwango kikubwa waliathiriwa na dhana za kikoloni na upendeleo wa kibepari kuwa Afrika ni bara la giza na la washenzi wasiokuwa na aina yoyote ya ustaarabu na walistahili kustaarabishwa na wazungu kupita mlango wa ukoloni.
                Nadharia ya Utaifa, imeasisiwa na S. Adeboye, Babalola, Daniel P. Kunene na J. P Clark. Katika nadharia hii wamejaribu kuondoa dosari ambazo nadharia zilizopita zimeshindwa kuondoa. Kutokana na kwamba wananadharia waliopita mara baada ya kutafiti hawakuwa tayari kuchapisha matokeo yao halisi ya utafiti bali kuyahariri matokeo yao. Na wanaona ni kosa kubwa kufanya utafiti bila kuwahusisha wahusika wa eneo la utafiti.                                               
 Hivyo ili kufahamu vyema historia ya fasihi simulizi ya kiafrika ni lazima kuhusisha wataalamu na wanazuoni wa taifa au jamii hiyo. Kwasababu wataalamu na wanazuoni hao ndiyo wenye ujuzi wa lugha, utamaduni na historia ya jamii hiyo.                                                              
  Kiujumla wananadharia ya kitaifa wanaamini kuwa chimbuko la fasihi simulizi ya kiafrika inapatikana ndani na jamii ya kiafrika na ili kuchunguza fasihi ya jamii husika sharti wataalamu na wanazuoni wa jamii hiyo wahusishwe.

3. Nadharia ya Hulutishi                                                                                                              Nadharia hii iliasisiwa na wanazuoni wa kiafrika wenye mtazamo kuwa hata wageni wamechangia sana katika kukuza taaluma ya fasihi ya kiafrika. Wananadharia hawa wanaona kuwa fasihi ya kigeni na ya kijadi zimeathiriana na kuingiliana. Miongoni mwa waasisi na watetezi wa nadharia hii ni pamoja na M.M. Mulokozi, Johnson, Ngugi wa Thiong`o, Chinua Achebe, Frantz Fanon, Abiola Irele, Taban Lo Liyong, n.k.  Hivyo basi historia ya fasihi simulizi ya kiafrika inaweza kujadiliwa kwa kuhusisha au kuchanganya mawazo ya wataalamu wote wa kigeni na wakijadi.                                                                                                                                     
 Wao walianza kuandika kazi za fasihi ambazo zinajaribu kuhusianisha ujadi wa Waafrika na usasa unaotokana na ujio wa wageni. Kwa mfano, Chinua Achebe katika Things Fall Apart, No Longer At Ease; Ngugi wa Thiongʼo katika The Grain of Wheat na Lo Liyong, T. (1972), Popular Culture of East Africa, Nairobi: (Longman Kenya) n.k. mtazamo huu umekuwa maarufu na kwa kiasi kikubwa bado unatumika. Hata utafiti wa Samwel unajaribu kuangalia ujadi wa majigambo na usasa.       
Hitimisho                                                                                                                                              Kwa ujumla nadharia zote tatu zimejaribu kuangalia chimbuko la fasihi simulizi na kutoa muelekeo kuhusu asili ya fasihi simulizi ya kiafrika. Kazi za fasihi zimeanza tangu binadamu walipoanza kuishi pamoja. Kazi hizo zilisimuliwa na kuaksi shughuli zilizokuwa zinafanywa na watu katika mazingira ya wakati huo. Kadri mazingira yalivyobadilika, hali kadhalika mambo yaliyosimuliwa yalibadilika. Kwa mfano, watu waliokuwa wanalima viazi, masimulizi yao yalihusiana na kilimo na matumizi ya viazi. Lakini baadaye watu hawa waliletewa mfumo wa kulima pamba. Kwa hiyo, masimulizi yao yalibadilika na kuelekea kwenye kilimo na matumizi ya pamba.                                                                                                                                                         
Vile vile waliotumia pinde na mishale katika uwindaji waliunda masimulizi yahusuyo maumbo na matumizi ya vifaa hivyo. Jamii hiyo ikipata na kutumia bunduki itabidi misemo na masimulizi yanayohusiana na bunduki.                                                                                                  
 Kwa hiyo fasihi simulizi ya kiafrika ilikuwepo hata kabla ya ujio wa wageni lakini ilianza kupata athari mara baada ya ujio wa wageni, athari na muingiliano wa fasihi simulizi hauoneshi kuwa fasihi imeanzia sehemu gani kwakuwa fasihi yoyote lazima iathiriwe na iathiri fasihi nyingine. Hivyo basi, kila jamii au taifa huwa na fasihi yake na utamaduni wake ambapo maingiliano ya watu na tamaduni zao huweza kuathiriana na hivyo kuathiri pia fasihi ya jamii husika.